Munishi
Group:
Members Posts: 78 Joined: Nov. 2003
|

"Maovu ya CCM sasa basi" Mwinjilisti Faustin
Munishi http://www.munishi.com/
CCM imeleta Jehanamu Tanzania. Watanzania watakaoingia Jehanamu,
Itabidi Mungu awapunguzie ukali wa moto kwani tayari wameungua
vya kutosha chini ya utawala dhalimu wa CCM. CCM ni wanyanganyi.
Walianza kuwanyanganya wananchi mali zao wakitumia azimio la
Arusha, na sasa Mkapa anatunyanganya mali akitumia ukusanyaji
wa kodi. Anatumia TIN kama nambari 666 ya mpinga Kristo kutunyanganya
mali zetu. Je Roho ya mpinga Kristo inafanya kazi ndani ya CCM?
Kila dalili zinaonyesha hivyo.
Wananchi wapendwa yangu ni machache sana leo. Maisha yetu na
watoto wetu ni muhimu kuliko chama chochote cha siasa. Hakuna
sababu ya kuwa mwanachama wa chama cha kisiasa, wakati chama
husika ndicho sababu ya kuharibika kwa maisha yetu ya sasa na
baadaye. Nazungumza kuhusu CCM. Inasikitisha kuona kwamba wananchi
Tanzania wameyazoea maovu ya CCM kiasi cha kukata tamaa ya kujikomboa.
Kwao maovu wanayofanyiwa ni kawaida iliyozoeleka, na hawaoni
sababu ya kufanya chochote kujitoa kwenye makucha ya CCM. Niko
hapa kuwapa sababu za kuanza harakati za kujikomboa. Tunataka
ukombozi kwa sababu ni haki yetu. Lazima tujikomboe kwani tusipofanya
hivyo hakuna atakayefanya kwa ajili yetu. Maisha yetu ndiyo
yanayoharibiwa, kwa hiyo hakuna mhadhiriwa nambari moja kama
mwananchi wa Tanzania. CCM inawatesa Watanzania, wengine inawaua
kosa lao ni kusema CCM itoke madarakani kwani sera zake zimeiharibu
Tanzania.
Maumivu Mateso Dhuluma Uonevu, na uchungu wote tunausikia, na
mwisho wa kuvumilia umefika. Kifo mara nyingi huwa ndio mwamuzi
kati ya uchungu na maumivu makali, huupumzisha mwili usiteseke
tena. Tusipochukua hatua kwa kuogopa kuuawa, mateso na maumivu
ya CCM yatafanya kile tunachokiogopa. Tayari yameua wengi, na
wengi wako mbioni kufuatia mkondo huo.
Swali langu kwenu ni hili: Mnataka CCM iue wangapi ndipo mseme
imetosha liwalo na liwe? Kwangu naona imetosha, SASA BASI. Liwalo
na liwe, tutachukua hatua za haraka kujikomboa. Je tuchukue
hatua gani? Kwamba tumefikia mahali pa kujiuliza swali hilo,
hiyo ni hatua nzuri ya mwanzo. Nani anayeweza kusema kwamba
mateso ya CCM hayajamhadhiri kwa lolote? Atakuwa anasema uongo.
Kila Mtanzania mdogo kwa mkubwa, ameonja maovu ya CCM.
Siyo nia yangu kuamsha hisia zenu kinyume na CCM bali nia yangu
ni kuwafanya muipende kiasi cha kuitoa madarakani. Kuitoa CCM
ndani ya mawazo yenu ni rahisi kama ilivyoingia. Swali la kujiuliza
ni Je CCM iliingizwaje kwenye mawazo na fikra zetu? Jibu lake
ndiyo njia ya kuitoa na kuisahau. Sitaki tufanye kosa la kuitoa
CCM kwa mbinu wanayoitumia kubaki madarakani. Tutakosea kwani
tutakuwa tukifanya kile wanachokijua zaidi yetu. Kwa hiyo mawazo
kwamba tutaitoa CCM kwa mtutu wa bunduki msahau.Tena hatuwezi
kutumia chama kingine cha siasa kuitoa CCM, kwani hakutakuwepo
na tofauti.
TUTAITOA CCM MADARAKANI BILA SIASA
" Siasa ni uongo, kwa hiyo hatuwezi kuutumia uongo kuwatoa waongo."
Siasa ni uongo, kwa hiyo hatuwezi kuutumia uongo kuwatoa waongo.
Ndugu wananchi, asiwadanganye mtu. Hakuna siasa nzuri. Wanasiasa
wote duniani mbinu zao zinafanana tofauti ni mahali mbinu hizo
zinapotumika. Kwa hiyo rais wa Amerika hana tofauti yeyote na
wanasiasa wetu hapa Tanzania sema kiwango cha uongo wanachotumia
wanasiasa wa nchi zilizoendelea kinazidi kile kinachotumiwa
na wanasiasa wa nchi zinazojaribu kuendelea.
Kifupi hakuna nchi iliyoendelea duniani.Kilichoendelea ni mbinu
za kuwaibia wananchi walio wengi mali yao ambayo ni haki yao,
na kuiingiza kwenye mkondo wa kisiasa ambao unalindwa na uongo
pamoja na silaha kali. Kwa hiyo mbinu ya kwanza kuwatoa CCM
madarakani ni kutambua kwamba wanasiasa wote duniani ni waongo.
Pili ni kutokusikiliza uongo wao ambao hupeperushwa na vyombo
vya habari kila siku. Ni vizuri mjue kwamba hakuna vyombo huru
vya habari katika dunia inayoongozwa na siasa. Kwa hiyo someni
habari magazetini, pia sikilizeni redio. Lakini mjue asilimia
tisini ya yale mnayoona na kusikia kwenye vyombo vya habari
ni takataka kama siyo uongo na mbinu za kuwafanya mnunue bidhaa.
Kwa sababu wanasiasa wengi siyo waandishi wa habari, kazi hiyo
hufanywa na wanataaluma hiyo kwa malipo.
Kwa hiyo hamtakosea kama mtasema kwamba waandishi wa habari
wameshirikiana na wanasiasa kuifikisha hali yetu kimaisha ilipo.
Uzuri wa waandishi wa habari, ni kwamba wanaweza kirahisi kurudiwa
na fahamu zao, na kuwageuka wanasiasa na kuungana na sauti ya
wanainchi. Tatizo ni kwamba walikuwa hawajui kama mnajua. Wakijua
kwamba nimewaambia na mbaya zaidi wajue kwamba sasa mnajua yale
waliyowaficha muda mrefu, watajikomba kuwaumbua wanasiasa. Hapo
tuwe tayari kusikia mengi. Watakapogeukana hiyo ni furaha tele
upande wetu.Tutakuwa tumempata msaidizi katika vita yetu ya
kuwatoa CCM madarakani.
WANASIASA HUTUMIA VYOMBO VYA DOLA KUWANYANYASA WANANCHI "Kila
inapobidi majeshi yote hutumika kulinda maslahi ya wanasiasa.
"
Siyo rahisi wanasiasa warudiwe na fahamu zao, hasa ukitilia
maanani kwamba wamezoea ukubwa na kutaka kuabudiwa kama 'miungu'
wadogo. Kwa hiyo watatumia kila mbinu kubaki madarakani. Mbinu
wanayoijua zaidi ni ile ya kutumia vyombo vya dola kama polisi
na majeshi yote ya angani nchi kavu na majini, bila kusahau
vikosi vya siri ambavyo hutumiwa kuwanyamazisha wapinzani.
KAZI IKO HAPA.
Wananchi wapendwa sipendi kuwaficha niwaambie kibarua kilicho
mbele yetu ni rahisi. Nitakosea sana nikifanya hivyo. Jukumu
langu ni kuweka wazi mbele yenu kila pingamizi tutakalokutana
nalo, na kuwaeleza mbinu na njia sahihi ya kupambana na adui
yetu. Majeshi yote yameundwa na wananchi wa TANZANIA. Polisi
kwa lengo la kulinda mali zetu wananchi, na majeshi yale mengine
wanasema lengo lao ni kulinda mipaka ya nchi yetu.
Hiyo ndiyo lugha wanayotumia wanasiasa kutuonyesha kwamba majeshi
yako kwa ajili yetu wananchi kumbe ni kinyume chake. Kila inapobidi
majeshi yote hutumika kulinda maslahi ya wanasiasa. Mnakumbuka
yaliyowapata wananchi wa Zanzibar walipojaribu kuipinga CCM.
Wananchi zaidi ya sabini walipoteza maisha yao, huku wengine
wakikatwa viungo vya miili yao ili kuwafundisha adabu.
Yaani watanzania wako tayari kuua wenzao kwa ajili ya wanasiasa.
Hiyo ndio kazi iliyo mbele yetu. Mjue kuna watu walio tayari
kuua kwa ajili ya CCM na viongozi wake. Na tayari walifanya
hivyo mchana jua linawaka bila kuogopa kamera za TV. Inataka
moyo, lakini msisahau nguvu iliyo katika KWELI. Ukweli utatuweka
huru mbali na wanasiasa waongo. Kweli ni NENO la Mungu ambalo
ndiyo silaha yetu yenye nguvu zote.
TIINI MAMLAKA HATA CCM?
"Tuna haki na uhuru wa kuikataa CCM, na Mungu aliyetupa hawezi
kutunyanganya haki na uhuru huo. Ni mali yetu, aliyetupatia
ni Mungu na tumeamua kutumia haki na uhuru huo kuikataa CCM
ya wauaji. "
Wacheni waje wakitumia silaha, sisi tutawakabili kwa NENO la
Mungu. Kwa imani yote yawezekana kwa waaaminio. Imani yetu kwa
Mungu tusikubali iyumbishwe na chochote. Siyo matisho ya CCM
wala kejeli zao.Mara zote wananchi ndio wengi kuliko risasi
zote CCM walizojilimbikizia. Sauti ya wengi ndiyo sauti ya Mungu.
Tukisema kwa sauti kubwa kwamba 'CCM CHAMA CHA MAJAMBAZI HATUKITAKI,'
hiyo ndiyo itakayokuwa sauti ya Mungu. Na hakuna awezaye kushindana
na MUNGU. Tuna haki na uhuru wa kuikataa CCM, na Mungu hawezi
kutunyanganya haki na uhuru huo. Ni mali yetu, aliyetupatia
ni Mungu na tumeamua kutumia haki na uhuru huo kuikataa CCM
ya wauaji. Watakaopingana na uamuzi wetu kuikataa CCM, hao ndio
watakaokuwa wakipingana na agizo la Mungu. Ndiyo watakuwa wameasi
mamlaka ya Mungu. Kwa hiyo lazima waitii mamlaka yetu wananchi,
kwani hiyo ameiweka Mungu mwenyewe. CCM iliwekwa na mtu mmoja,
ni sawa ikitolewa na watu.
Walitudanganya kwamba wanafanya uchaguzi ili iwe kana kwamba
iliwekwa na watu, lakini tumegundua janja yao.Maoni ya wengi
hayajawahi kuheshimiwa katika uchaguzi wowote ule tuliowahi
kuwa nao. Kwanza tulikuwa tukichagua nini kinyume cha nini?
Uchaguzi lazima uwe kati ya Shetani na Mungu, na siyo kati ya
shetani na mashetani. Chaguzi tulizowahi kuzifanya kabla ya
vyama vingi vya siasa, zilikuwa kati ya Shetani na kivuli. Chaguzi
tulizofanya wakati wa vyama vingi vya kisiasa, zimekuwa kati
ya Shetani {CCM}na vijishetani {vyama vya upinzani} ambavyo
navyo vitakua kumfikia Shetani mwenyewe. Sasa tunataka uchaguzi
wa kweli. Tuchagua kati ya Shetani na Mungu. Duniani hakuna
uchaguzi zaidi ya kuchagua MUNGU na Shetani. Hakuna kitu cha
tatu wananchi msidanganyike.
GIZA NA NURU
" Msije mkanilaumu kwamba nilisema siasa ni dini ya shetani."
Dunia imekuwa na historia ya kupenda giza kuliko NURU, ndio
maana wengi wanapenda siasa ambayo ni giza nene. Nuru ya injili
sasa inaangaza duniani kote. Inatufundisha kuikataa siasa ambayo
hutumiwa na shetani kuyatekeleza malengo yake ya kuharibu, kuchinja
na kuua. Msije mkanilaumu kwamba nilisema siasa ni dini ya shetani.
Lakini hata kama ulimi wangu ungeteleza niseme hivyo, ningekuwa
nimekosea nini? Je sasa nimesema hivyo? Hapana. Nilichosema
ni kwamba siasa ni chombo anachotumia sana Shetani. Hatuwezi
kumkataa Shetani na kuikubali SIASA chombo anachokitumia. Tumkatae
jongoo na mti wake. Wananchi! Siasa ni mbaya na hilo mnalijua
fika. Wengi mtaniuliza nini mbadala wa siasa? Jibu langu ni
KWELI. Neno la Mungu ndiyo KWELI.
UJAMAA NA UBEPARI
"Ujamaa ulisikika mzuri masikioni, lakini kwa sababu aliouleta
alikuwa Nyerere mwanasiasa muongo, kila kilichovutia hakikutekelezeka."
Watu tofauti kwa nyakati tofauti wamekuwa na mawazo tofauti
kuhusu mfumo gani unaofaa kumwongoza mwanadamu. Wengine waliufuata
mfumo wa ukomunisti kama akina Nyerere, wakashindwa kabisa.
Mbaya zaidi walitumia miaka zaidi ya 30 kuyajaribu mawazo yao
ya ujamaa Tanzania. Matokeo yake yalikuwa kuiacha Tanzania ikiwa
imeharibiwa na sera zao mbovu, na hata sasa hatuna sera kamili
tunayoifuata.
Tanzania siyo mabepari wala siyo wajamaa kama alivyotaka Nyerere.
Sisemi ubepari ni bora kuliko ujamaa, kwani sera zote hizo ni
za kisiasa. Kwangu zote ni mbovu kwani zinakosa KWELI ndani
yake. Ujamaa ulisikika mzuri masikioni, lakini kwa sababu aliouleta
alikuwa Nyerere mwanasiasa muongo, kila kilichovutia hakikutekelezeka.
Badala ya aliyeanzisha kukiri kwamba alikuwa amesema uongo,
alitumia uongo mkumbwa kuutetea uongo mdogo aliouanzisha. Miaka
ikapita na tulichoambulia watanzania ni umaskini wa kutisha.
Nyerere alitutaka tuamini kwamba dunia yote inapita kwenye matatizo
kama yetu watanzania, na wakati huo huo polisi waliwakamata
wananchi waliopatikana na sabuni, dawa za meno na mafuta ya
kupikia kutoka Kenya. Ilikuwa ni sawa na kukamatwa na madawa
ya kulevya. Wengi wakati huo tuilijiuliza: Ikiwa dunia yote
ina mateso kama yetu, mbona hapa Kenya wao wanaogea sabuni?
Tofauti na sisi tunaotumia maziwa ya mpapai kuogea? Tena mbona
wenzetu wanatumia dawa za meno wakati Nyerere anaziita anasa?
Kweli kuogea sabuni ya REXONA au kutumia dawa ya meno ya COLGET
ni anasa? Nyerere mwanasiasa muongo alitutaka tuamini hivyo.
Wengi walimuamini na mpaka leo hawataki makuu. Waliukubali umaskini,
na hawataki kuchukua hatua zozote kupambana nao. Japo Nyerere
alisema adui zetu ni umaskini ujinga na maradhi, alitufundisha
kuwapenda na kuwakubali maadui hao. Nasikitika kusema kwamba
kuna watu waliomwamini Nyerere kinyume cha Amin wa Uganda. Waliomwamini
Nyerere walikosea sawa na waliomwamini Amin. Watu hao wawili
walileta madhara kwa nchi zao, lakini ya Nyerere Tanzania yalizidi.
Ninachotaka kusema ni kwamba mifumo yote ya siasa ilishindwa.
Sasa tuufuate mfumo wa Injili ambao hauwezi kushindwa. Injili
ni uwezo wa Mungu, sioni haya kusema Injili ndio mkombozi wa
dunia. Itaikomboa dunia kutoka katika minyororo ya uongo ya
wanasiasa. Lazima tuiamini Injili kama kweli tunataka ukombozi.
Dunia ni ya Mungu na haiwezi kuongozwa kwa siasa za watu ambazo
ni uongo. Dunia itaongozwa na KWELI ya neno la MUNGU.
WANASIASA NA MFUMO WA BIASHARA NCHINI
"Inasikitisha kuona wananchi ndani ya nchi yao wakiteseka, huku
wanasiasa na wageni wachache wakimiliki njia zote kuu za uchumi."
Duniani kuna vita nyingi na tetesi za vita. Yote hayo ni matunda
ya wanasiasa. Shetani anawatumia kuua na kuharibu maisha ya
watu. KWELI imekuja ili tuwe na uzima, kinyume na shetani aliyekuja
kuua. Utajiri wa dunia uko mikononi mwa wanasiasa. Mnajua ni
kwa nini? Ili utajiri huo utumike kununua kila wanachokihitaji.
Nanyi wananchi ni moja ya bidhaa ambayo wanasiasa hupanga kuinunua.
Mnanunuliwa wakati wa kura ili kutia saini chaguzi ambazo washindi
hujulikana kabla ya siku ya kura.
Hawataki mjiendeleze ili muwe rahisi kununuliwa. Ndio maana
wengi wenu hamjiwezi kimaisha na hiyo haiwasumbui wanasiasa
kwani wanapenda mbaki kama mlivyo ili wawatumie. Hata wale wanaojaribu
kujipatia riziki zao za kila siku kwa kuanzisha biashara ndogo
ndogo, bado wanasiasa hawaachi wafanye hivyo. Kila siku tume
ya jiji hupewa kazi ya kuusafisha mji, na wafanyabiashara ndogo
ndogo ndio uchafu unaotakiwa kusafishwa mijini. Siyo ajabu kwani
huo ni mpango kamili unaolenga kuwanufaisha wafanyibiashara
waliounganishwa kisiasa. Hawa ndio wale ambao hupewa tenda za
serikali ili wagawane mapato na wanasiasa.
Kuna wengine wa asili ya kiasia ambao nao hupewa kumiliki maeneo
yote muhimu ya kibiashara. Makubaliano ni kwamba mapato wayagawane
na wanasiasa. Inasikitisha kuona wananchi ndani ya nchi yao
wakiteseka, huku wanasiasa na wageni wachache wakimiliki njia
zote kuu za uchumi. Hali hii haipaswi kuwa hivyo. Wananchi wanatakiwa
wapewe uhuru wa kufanya biashara popote katika nchi yao. Udogo
wa biashara usiwe ndio sababu ya kumsumbua mwananchi, kwani
hata hizo biashara kubwa ziliaza zikiwa ndogo. Wananchi wanaoiamini
KWELI wanatakiwa waruhusiwe kufanya chochote chema katika nchi
yao.
Hali hiyo ndio itakayochochea ubunifu utakaopelekea kugunduliwa
kwa vitu vingi kwa ajili ya maisha ya kila siku ya mwanadamu.
Ugunduzi huo ndio unaoweza kuinua uchumi wa nchi husika kinyume
na nchi nyingine, kwani "akili ni nywele na kila mtu ana zake."
Na wale wanaogundua vitu, wanapaswa kulipwa sawa sawa na ugunduzi
wao. Hapo taifa litakuwa limejitengenezea wanasayansi wake,
wanaoweza kuvumbua vitu ambayo wengine hawana, na wakiviitaji
taifa linapata pesa za kigeni kuinua uchumi wa nchi.
Sekta ya elimu nayo itakuwa imeboreshwa kwani elimu kwa watoto
wetu itazingatia zaidi vitu tulivyogundua wenyewe, kinyume na
elimu ya sasa ambayo misingi yake ni mengi yaliyofanywa na wengine,
huku tukipima uwezo wetu katika kuyaiga. Ndiyo maana maisha
ya waalimu katika nchi nyingi ni duni. Wanasiasa hufundishwa
na waalimu, lakini kimaisha wametofautiana sana. Waalimu mishahara
yao ni midogo sana kulinganisha na wanasiasa ambao kila kukicha
hujiongezea mishahara na marupurupu mengi.
Katika nchi ambayo inaongozwa na KWELI bila siasa, waalimu ndio
wanaotakiwa kupata mshahara wa kuwatosha kumudu maisha yao kama
siyo uliowazidi wanasiasa. Hata kama watawazidi wanasiasa kimshahara
kuna ubaya gani? Hilo ni swali tu. Msije mkasema niliwaambia
mishahara ya waalimu izidi ya kila mtu. Lakini waalimu ndio
humfundisha kila mtu. Sasa inakuwaje kila mtu anampita mwalimu
kimshahara? Hapo nimetoka maana naona maswali hayaishi kichwani
mwangu. Mengine mtajijazia wenyewe. 
RAIS BILA WALINZI?
Watalinda nini wakati KWELI inajilinda yenyewe?
KWELI na uongo ni kama mafuta na maji. Huwezi kuvichanganya
hata kama utajaribu kufanya hivyo. Kweli inajilinda yenyewe
na haihitaji kulindwa na silaha kali. Uongo lazima ulindwe kwa
kutumia silaha kali, kwani hawajui wale waliodanganywa wakierevuka
watafanya nini. Ndio maana dunia nzima inafikiria kuhusu silaha
kali kuliko chakula cha wanadamu wanaoikaa. Waangalie wanasiasa
wanavyolindwa. Watu zaidi ya mia moja hawafanyi kitu kingine
duniani ila kumlinda mwanasiasa.
Naheshimu kila taaluma ya mtu, lakini siwezi kumshauri yeyote
awe mlinzi wa mwanasiasa. Kwa nini ufe kwa ajili ya uongo ambao
hukuusema? Tena kwa mshahara gani basi? Yaani wenzio wako ndani
wanakula vinono nawe unaungua jua nje? Sawa ni kazi yako. Unaipenda.
Sina la kuongeza. Lakini ikiwa mimi ndiye nitakayekuwa kiongozi
katika nchi itakayokuwa ikiongozwa na KWELI bila siasa, basi
sitaki walinzi. Watalinda nini wakati KWELI inajilinda yenyewe?
Unamkumbuka mmoja wa wanafunzi wa Yesu aliyejaribu kufanya kazi
ya kumlinda? Alikata sikio la mmoja wa askari waliokuwa wanamkamata
Yesu. Aliambiwa aurudishe upanga wake kiunoni kwani YESU ni
KWELI iliyotoka kwa Mungu na hakuhitaji kulindwa na mapanga
au bunduki. Pesa wanazotumia wanasiasa kununulia silaha za kujilinda,
zinatosha kumaliza baa la njaa duniani kote.
Yaani nina maana kila mtu duniani anaweza kula milo mitatu kwa
siku. Tena chakula kizuri. Lakini pesa zote wanatumia wanasiasa
kununulia silaha kali za kujilinda na wale waliowadanganya.
Mwisho wao umefika. KWELI itawatoa madarakani bila kutumia silaha.
Ole wao. Silaha walizojiwekea watazifanyia nini? Mbinu za vita
zimebadilika. Hatutatumia mbinu walizozizoea.
Nguvu ya kweli ya INJILI itawakata makali yao. Injili ni NENO
la Mungu ambaye ndiye KWELI yenyewe. Je wanasiasa watashindana,
au kupigana na Mungu? Kila la kheri katika vita yao hiyo. Watatoweka
mmoja baada ya mwengine. Hawatajua ilikuwaje, wala hawaruhusiwi
kujua. Pesa na utajiri havitawasaidia wakati huo. KWELI haipimi
uzito wa mtu kulingana na vitu alivyo navyo. Mtu ni mtu hata
kama hana vitu. Mtu huunda vitu, lakini vitu haviwezi kuunda
mtu. Vitu ni kwa ajili ya mtu, lakini siyo mtu kwa ajili ya
vitu.
WANASIASA HUTUMIA DINI KUTAWALA
Makanisa mengi yameanzishwa na kufadhiliwa na wanasiasa kwa
kwa lengo la kuyatumia kisiasa, wakati lugha yao ni kwamba chama
na serikali havina dini.
Dini ni imani kwa Mungu wakati siasa ni imani kwa watu. Zote
mbili ni itikadi zinazohitaji watu kufanikisha malengo yao.
Ndio maana nawataka watu wa dini zote tuungane pamoja kuitoa
siasa madarakani. Suala kwamba dini gani itatawala hilo lisitusumbue
kwa sasa. Muhimu ni wote tutambue kwamba wanasiasa wanatutumia
vibaya. Baada ya kutambua hayo tuachane kabisa na siasa. Kitakachofuata
ni kila dini inayowania uongozi kujitokeza hadharani na kutangaza
nia yao ya kutaka kuongoza. Wananchi wa dini husika, pamoja
na wale wasio na dini, bila kuwasahau wale wa dini nyingine
watakaoamua kujiunga na dini yenye sera nzuri kutoka kwa Mungu,
Watachagua dini gani iongoze kwa kipindi kilichozoeleka cha
miaka mitano.
Baada ya miaka mitano tutachaguana tena. Pamoja na kwamba kila
dini itakuwa na katiba yake, lakini lazima tuwe na katiba moja
ya pamoja. Nayo ni ile itakayozingatia Imani kwa Mungu ambayo
ndilo lengo la kila dini. Pamoja na kwamba dini fulani itachukua
uongozi kwa kipindi cha miaka mitano, bado kila dini itawakilishwa
katika baraza la makuhani ambalo ndilo litakalohusika na kuhakikisha
kwamba amri kumi za Mungu zinafuatwa kikamilifu. Kwa hiyo hofu
kwamba kutatokea michafuko ya kidini msahau kabisa. Badala yake
dini zote zitaingia katika ushirikiano ambao haujawahi kuonekana
tangu kuumbwa ulimwengu. Bado kila dini itakuwa huru kuendelea
kufanya mambo yake yenyewe, bila kuomba kibali kwa wanasiasa
kama ilivyo sasa.
Hakutakuwepo na makanisa ua misikiti inayodhaminiwa na serikali.
Makanisa mengi yameanzishwa na kufadhiliwa na wanasiasa kwa
kwa lengo la kuyatumia kisiasa wakati lugha yao ni kwamba chama
na serikali havina dini. Mambo yako hivyo karibu kila dini.
Inasikitisha kuona kwamba wengine wanafikia mahali pa kudanganya
kwamba watu wamepona kwenye mikutano yao ya kidini, kumbe ni
waongo. Tayari tumewangundua kuwa ni wapambe wa CCM. Wanalindwa
kama wanasiasa na huku wanajiita maaskofu. Wanatembelea magari
ya kifahari na huku waumini wao ni masikini wanaodanganywa kwamba
wakitoa watabarikiwa. Tayari viongozi wa dini wanawasaidia wanasiasa
katika kuendeleza ukandamizaji na uonevu kwa waumini wao, ili
mradi tu waitwe ikulu na wapewe magari na pesa. Hawana tofauti
na wanasiasa tunaotaka kuwatoa madarakani. Kweli ya Mungu ni
taa. Ikiwamulika, matendo yao yataonekana na kila mtu. Hawa
ndio watakaokwenda pamoja na wanasiasa wakati dini ya kweli
itakapochukua madaraka.
MAUAJI YA KISIASA SIRI YAFICHULIWA
Wanasiasa kwa makusudi wameziharibu taasisi zote. Duniani taasisi
zote hufanya kazi kwa ajili ya wanasiasa. Nchi zilizoendelea
wameendelea katika kujaribu kuficho hilo lakini nchi zetu jambo
hilo liko wazi. Kwamba wana mbinu kali za kulificha, haiwatofautishi
na wenzao katika nchi zinazoendelea. Inabaki kwamba kila taasisi
duniani inalinda maslahi ya wanasiasa kwanza. Mahakama mara
nyingi zinaonekana kupindisha ukweli, hasa pale ambapo mwanasiasa
anahusika. Hebu fikiri kuhusu gari lililotekwa nyara katikati
ya mji.
Watekaji wanamlazimisha mwenye gari kuliendesha kuelekea wanakotaka.
Baada ya safari ya kama kilomita mbili hivi, wanaacha gari la
kwanza baada ya kulizinga jingine kwa mbele. Mwanye gari la
pili anapigwa risasi na kuuawa hapo hapo baada ya kisichojulikana
kuendelea kati ya watekaji na yeye. Wanayaacha magari yote mawili
hapo baada ya kumwamuru mwenye gari la tatu kutoka ndani ya
gari lake na kuwapa funguo. Wanaondoka na gari huku wakiwaacha
wenye magari wote mahali pamoja, lakini mmoja ni marehemu na
mwingine amebaki bila gari.
Baada ya dakika kama tano hivi, Polisi wanawasili mahali hapo.
Wakiwa katika kuwahoji wenye magari wawili, waandishi wa habari
wa magazeti TV na Redio wanawasili mahali pa tukio. Usijali
wataulizana nini hapo, lakini sikiliza redio na utizame TV jioni,
halafu usome magazeti asubuhi yake. Utakayemsikia akitajwa kwamba
aliuawa na majambazi waliojaribu kumpora gari, ndiye aliyekuwa
amelengwa na taaluma zote hizo. Yaani habari yenyewe itasomeka
hivi. MAJAMBAZI WAMUUA BWANA XXXX Aliyekuwa mhubiri wa INJILI
bwana XXXX amefariki dunia baada ya majambazi kumfyatulia risasi.
Wakiongea katika sehemu ya tukio, bwana JJJJ na bwana SSSS walisema
kwamba walishuhudia majambazi wakimfyatulia risasi bwana XXXX
baada ya mvutano ulioonekana kama Bwana XXXX alikataa kuwapatia
majamabzi fungua za gari lake. Wakisimulia saidi kisa hicho,
walisema kwamba walisikia mlio wa risasi mara mbili, na baadaye
majambazi walitoka kwenye gari la huyo aliyekuja kujulikana
baadaye kama Bwana XXXX. Walimwamuru Bwana SSSS atoke kwenye
gari lake na awape funguo. Alitii, na majambazi waliondoka na
gari lake ambalo mpaka sasa halijapatikana. Kwa sababu vyombo
vyote vya habari vimelipa uzito suala hilo kwenye kurasa zao
za kwanza, wananchi wanaiamini hadithi hiyo. Ndiyo lengo lilikuwa
ifanyike hivyo ili wananchi waaminishwe uongo. UKWELI wa mambo
ni kwamba bwana XXXX alikuwa mlengwa kwenye sakata yote hiyo.
Kuna mtu aliyejua kwamba atapitia barabara hiyo saa hizo baada
ya kutafiti nyendo zake kwa zaidi ya miezi mitatu. Taasisi zilizotumika
kuwadanganya wananchi nazo zilihusishwa wengine wakijua na wengine
bila kujua. Walioporwa magari yao ndio ambao hawakujua nini
kilichokuwa kikiendelea. Ilikuwa hivi: Bwana XXXX aliwaudhi
wanasiasa kwa kujaribu kuwaambia kwamba wanasiasa hawawatendei
mema wananchi walio wengi. Walipochukizwa naye wakaamua kwamba
atauawa. Pesa nyingi zikatolewa kwa ajili ya kazi hiyo. Walitakiwa
watu kutoka katika taasisi mbili nyeti. Polisi na vyombo vya
habari vilitosha kukamilisha zoezi zima.
Kachero mmoja wa polisi alitumika kuzijua nyendo zote za Bwana
XXXX, halafu mkuu moja wa kituo cha polisi alitakiwa kuwatoa
vijana ambao watafanya kama wafanyavyo majambazi. Na huyo huyo
ndiye aliyetakiwa kuvipigia simu vyombo vya habari kuviarifu
kuhusu tukio, na jitihada zao za kuwafukuza majambazi.
Lengo likiwa kutekeleza mauaji ya kisiasa, na kuyafanya yaonekane
kama ujambazi wa kawaida. Walikosea. Kwanza hakuna ujambazi
wa kawaida. Kwamba kuna ujambazi hiyo inaonyesha kushindwa kwa
wanasiasa kuwalinda wananchi pamoja na mali zao. Pili: Kwamba
wanamuua mtu kwa sababu tu amewakosoa chama tawala CCM huo ni
wendawazimu nambari ONE. Wananchi mfano huu unaonyesha jinsi
wanasiasa wanavyoweza kuzitumia taasisi kuyaficha maovu yao.
Hii ni siri iliyofichuliwa katika mijadala ya Internet huko
BCSTIMES .COM baada ya siri hii kufichuliwa na mtu aliyejiita
AISHA AIESHI. Unaweza kujisomea mwenyewe kisa hicho kwa KUBONYEZA
HAPA. Kuna matukio mengi ya zamani na hivi karibuni yanayofanana
kabisa na mfano huu. Mauaji ya watu zaidi ya sabini kule Zanzibar,
Kifo cha SOKOINE aliyekuwa waziri mkuu wakati wa Nyerere. Kifo
cha KOMBE aliyekuwa mkuu wa kikosi cha usalama wa taifa wakati
wa Nyerere, na wengine wengi.
Mchungaji Faustin Munishi ambaye pia ni mwimbaji maarufu wa
nyimbo za injili Afrika ya mashariki na kati, ametangaza azma
yake kuwania kiti cha urais Tanzania katika uchaguzi ujao. Mengi
yamesemwa kuhusu hatua ya mchungaji huyo, na hapa ni sehemu
ya mjadala katika mtandao. Inasemekana serikali ilikuwa imeufungia
mjadala huu usiweze kusomwa na Watanzania. Gazeti la Injili
kwenye internet linakuletea mjadala huo bila kuhariri chochote.
SASA BASI INATOSHA 
Ndugu wananchi yangu yalikuwa hayo machache. Msimame imara,
wala msikubali kuyumbishwa na hawa wanasiasa. Mkatae kabisa
mbinu zao za kutaka kuendeleza maovu yao kwa kuachiana viti.
Nyerere alituachia MKAPA ili alinde madhambi yake.Naye Mkapa
anataka kutuachia sijui nani ili alinde madhambi yake. Watalindana
mpaka lini? Mwisho wao umefika.Sasa tunataka dunia isiyo na
kitu kinachoitwa SIASA.
Wametudanganya vya kutosha, wakatuibia vya kutosha sasa tunataka
KWELI ya neno la Mungu iongoze Tanzania. Mungu ni pendo na anaipenda
Tanzania ndio maana amenituma mtumishi wake kuwaletea ujumbe
huu. Msijali kufurukuta kwao kwani wangefanyaje nao wanakata
roho? Watawapeleka kwenye madanguro yao kuwatesa lakini msikate
tamaa. Watatumia kila mbinu ikiwepo ya kuwafungulia kesi za
uongo, msijali kwani hayo yote hayana budi kuja. Nguvu ya dola
ni ndogo sana ukilinganisha na nguvu ya wananchi wamoja.Umoja
wetu na imani yetu kwa Mungu ndiyo silaha kubwa ambayo kila
mmoja wetu lazima awe nayo.
Watahangaika kujua nani anayetupa nguvu tulizo nazo, lakini
jibu watakalolipata litawarudisha hatua mia tatu nyuma. Wataanzisha
magazeti kwa lengo la kuueneza uongo wao lakini watagonga mawe
kwani wananchi tumeyashitukia magazeti ya hivyo. Watatumia pesa
walizoiba kwetu kutununua kwazo, nasi tutatumia pesa bila kuwaunga
mkono.Pesa ni zetu. Zikirudishwa hatuachi. Tutazitumia. Tuanze
mara moja zoezi la kuchoma moto kadi za vyama vya kisiasa. Sisi
ni waumini wa dini na hiyo inatutosha. Hatuwezi kuamini katika
dini mbili, yaani siasa na INJILI. Moja ni ya shetani na nyingine
ni ya Mungu.Sisi tumeamua kuwa upande wa Mungu. Mungu hawezi
kutuacha watoto wake tuteswe na siasa za yule mwovu.
Hatua ya kwanza tutakayoichukua kuelekea ukombozi, Mungu atachukua
hatua mia moja kutulinda na CCM pamoja na wanasiasa waovu. Mara
zote Mungu hafanyi chochote kutulazimishia matakwa yake. Lakini
tunapoamua kwamba tutaifuata njia hii, na kisha tuombe baraka
na ulinzi kutoka kwake, mara moja Mungu hutujibu maombi yetu
kwa kuanza kutulinda na kutupa ufunuo zaidi. Nilipochukua kalamu
kuanza kuandika haya, ndipo ufunuo wote huu uliponijia kutoka
kwa Mungu. Ningengoja ufunuo kwanza ndipo niandike, pengine
mpaka mwaka 2080 ndipo ningepata ufunuo huu. Ni muhimu sana
kutilia maanani ujumbe huu. Huwezi kuusoma popote kwani lengo
kubwa la serikali ni kuwazuia wananchi kujua. Wanajua kwamba
mkijua mtawauliza maswali wasiyopenda kuulizwa. Wana mengi ya
kuficha na anayejaribu kuyafichua ni adui wao nambari moja.
Kama hawatammaliza kibiashara au kisiasa, basi watapanga njama
za kuutoa uhai wake. Wameuawa wengi ndiyo maana hatuchukulii
kama mzaha matisho yao ya kuua. Bonyeza hapa usome yale waliyokusudia
kumfanyia mwandishi wa hotuba hii.[/B][B]
Mchungaji Faustin Munishi.
|